Muziki Ulimpenda BEN POL, Mapenzi ya MREMBO Kenya Yamempenda zaidi...

BEN Pol bila muziki na kuwa staa, angeingiaje kwa mrembo wa kishua, Anerlisa Muigai? Mtoto ‘mkare' halafu ana kisu kikali, wazazi wake pia wana mawe ya kutosha.

Ukiwa mwanamuziki mzuri huwezi kukosa wanawake wazuri wanaokuzunguka na kukutolea udenda. Ben ni mwanamuziki fundi. Ana uwezo mkubwa. Kama unabisha njoo tubishane.

Ben ameshashinda sana kwenye muziki wake, ana bando lililosheheni ngoma kali. Ukinipa santuri yenye ‘misongi' yote ya Ben, nakuhakikishia sita'skip wala ku’forward. Zote ni tamu mwanangu!

Unanipaje mtihani wa kusikiliza “Jikubali” halafu niache “Bado Kidogo”? Utanikuta nimeshasikiliza zote, halafu hutanifanya chochote. Masikio ni ya kwangu.

Unakuja na mitego yako, eti unaniambia nichague kati ya “Pete” na “Maneno”, nakupa taarifa mapema kuwa nitatazama zote. Hulipii kodi macho yangu, ebo!

Leta nyingine na nyingine kutoka kwa Ben, janki wa ugogoni hana kazi mbovu. Tangu Nikikupata, Samboira, Phone, Why, Wapo na nyingine zote unazozijua, mimi kaka yenu nimeshapitisha kuwa Ben hana kazi famba. Uzuri yeye mwenyewe anajijua.

Kwanza unajua nini? Uwezo wa Ben hauhitaji kutetewa. Unajitetea wenyewe. Kwa kazi za kiwango bora ambazo ameshafanya, kujitokeza kutetea kipaji cha Ben sio umbea huo? Nami sitaki kusutwa na uzee huu!

Himaya ya Harambee, palepale kwa Baba Muasisi, Jomo Kenyatta, Ben alipeleka ushababi wake, akang'oa mrembo, kilichofuata dogo amesahau tena muziki.

 LABDA nakwenda kasi sana, hebu nipunguze mwendo; haijawahi kubadilika kuwa hakuna bidhaa ambayo huvuka boda kwa urahisi kama muziki. Muziki hauna mipaka arifu!

Na hiyo ikawa sababu ya Ben kuwa mwenyeji Kenya. Si unajua mwanamuziki? Popote muziki wake unapofika, yeye ni nyumbani. Hupata mashabiki na jukwaa.

Janki wa ugogoni alikwenda Kenya na muziki wake, alipofika akanasa na mapenzi. Halafu unajua nini, mapenzi yakawa yenye cheo, maana aliyemnasa ni mrembo tajiri, ambaye baba na mama wote mambo safi.

Yaleyale ya Ngoswe, dunia haijabadilika na kanuni ni ileile “penzi kitovu cha uzembe”, siku hizi Ben muziki sio kipaumbele, mkazo wake kwa sasa ni kulinda penzi kisha bata kwa sana.

Tangu Dubai, akatinga kwenye mgahawa wa Nusr-Et ambao huhudumia mastaa wa dunia. Tokea alipokula nyama choma iliyokatwa na bwana mahoteli supastaa wa Kituruki, Nusret Gokce ‘Salt Bae', ambaye alishawakatia minofu akina P Diddy, Lionel Messi, Maradona, Paul Pogba na wengine, Ben amebadilika sana. Haonekani akiwazia ukuaji wa muziki wake.

Juzi hapa alikuwa Marekani, akaitalii Greater Downtown Miami kwa chopa. Ratiba ya sasa ya Ben imesheheni matukio ya kula bata na kumsindikiza girlfriend wake kwenye mishe zake za biashara, kuliko mitikasi yake ya kimuziki.

Come on Ben, yule mtoto wa Ukikuyuni, asingedata kwako kama sio muziki. Sina maana amekupenda kwa sababu wewe ni staa na ni mwanamuziki, hapana, don't quote me wrong, kid!

NAMAANISHA bila muziki kukunyanyua Ben, huyo Anerlisa ungegongana naye viwanja vipi? Majengo au Makole? Mrembo mwanamitindo, corporate businesswoman. Familia yao inainywesha Kenya ulabu kwa asilimia 20.

Hapo maana yake nini? Moja ya tano ya pombe yote inayonyweka Kenya, inazalishwa ukweni kwa Ben. Kiwanda cha Keroche Breweries kinachomilikiwa na wakwe wa Ben, ndio kinalewesha Wakenya kwa asilimia hizo.

Pamoja na kwamba Anerlisa anatoka katika familia hiyo, naye anapiga mishemishe heavyweight, anamiliki kampuni ya Nero Limited ambayo inamiliki kiwanda kinachozalisha maji ya Executive Still na Life Still.

Hivyo, Anerlisa ni maana halisi ya mtoto wa kishua. Hivi sasa ni CEO wa Nero Limited, halafu ni CEO ajaye wa Keroche Breweries. Kwa sasa CEO wa Keroche ni bi mdashi wake, Tabitha Muigai, dingi wake, Joseph Karanja ndiye Chairman.

Umenimanya? Ben kaopoa mtoto wa koo ya wenye hela. Ndio maana siku hizi hataki kusumbuana na akina Lucci na Manek kutoa ngoma mpya. Maisha yanataka pesa, naye amelenga na shabaha zimempa matokeo. Yeye sasa ni bata tu!

NGOJA NIMUWEKE KITAKO!

Ben ni mdogo wangu, namuogopa kwani mpaka nikamtete kwa majirani? Namuweka kikao hapahapa! Sikiliza Ben, Keroche Breweries na Nero zinamhusu Anerlisa, sio wewe. Do you get that, son?

Mkishafunga ndoa hapo sawa, maana hata ukipigwa chini unaweza kujiliza upate mgawo, lakini kwa sasa wewe sio lolote kwenye biashara za wakwe zako na girlfriend wako.

Wewe wako ni muziki na ndicho unapaswa kuendelea kukomaa nacho. Sisi kaka zako, of course na dada zako wote Bongo, wameniachia jukumu la kukwambia hivi; ole wako ulowee ukweni.

MUZIKI wa sasa unakwenda kiteknolojia. Mwanamuziki anahitaji mtaji mzuri wa kifedha na timu ya masoko ya kimtandao, aweze kuufikisha mbali muziki wake.

Ben badala ya kutumia pesa za Anerlisa kuzunguka dunia akila bata, ni wakati wake wa kujenga mtandao mzuri wa kibiashara. Awe na timu ya kuufikisha mbali muziki wake. Afanye kolabo na wanamuziki wakubwa Afrika na duniani.

Sisi tunafahamu kuwa Ben ni mkali tangu na tangu, lakini alibaki kuonekana mediocre kwa sababu hakuwa na mtaji wa kijitangaza. Anerlisa amemdondokea, yeye anaamua kula starehe kuliko kazi. Mbona sisi Wagogo hatupo hivyo? Tabia hiyo ameitoa wapi?

Ben ni shamba linalotoa malighafi muziki, nayo malighafi ikishaingia studio (kiwandani), bidhaa (muziki) hutokea. Ben ni rasilimali yenye kutosha kuendesha kampuni kubwa.

Sisemi akamlilie Anerlisa ampe pesa, no, sisi Wagogo hatupo hivyo. Ni ushauri kwake kwamba anaweza kujenga kampuni yenye wanahisa wawili, yeye na Anerlisa. Akakuza mtandao mkubwa wa muziki, matokeo makubwa yakafuata.

Yule dogo bwana! Tulimpeleka Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), ni msomi mjue yule! Msomi wa IFM anapaswa kuwa mjanja sana linapokuja suala la fedha, lakini yeye anakwenda kupiga mbonji Kenya. Anazingua big time!

Matokeo yake hapa Bongo, Harmonize anaonekana msanii mkubwa kuliko Ben, what an insult! Ben alipomshirikisha Harmonize kwenye “Why”, ngoma iliwekwa YouTube kwenye akaunti ya Harmonize.

Ni kwa sababu Harmonize ana msuli mkubwa YouTube kuliko yeye. Na hayo ni matunda ya lebo yake iliyopita kumtangaza. Naye ana nafasi ya kufungua milango iliyofungwa, lakini anatuletea mambo ya ngoswe. Hataki kufanya kazi. Nasikia siku hizi hata Kiswahili anaongea cha Kikenya.

Ndio maana Harmonize na Shetta waliamua kumuibukia Anerlisa na kumtongoza, wakati wanajua ni shemeji yao, labda waliona kwenye miti hakuna wajenzi.

Alamsiki.

Ndimi Luqman MALOTO

Comments

Popular posts from this blog

JINSI YA KUMFANYA MWANAMKE AKOJOE HARAKA WAKATI WA TENDO

JINSI YA KUMKOJOLESHA MWANAMKE KWA HARAKA

JINSI YA KUMFANYA MWANAMKE ASIKUSAHAU KATIKA TENDO LA NDOA