Mtuhumiwa wa uhalifu wa kivita afariki Ujerumani



Kiongozi wa zamani wa waasi wa Rwanda amefariki dunia akingojea kusomwa upya kwa kesi yake nchini Ujerumani, baada ya kutiwa hatiani kwa uhalifu wa kivita uliotendeka katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo takribani muongo mmoja uliopita.

 Ignace Murwa-na-shyaka, mwenye umri wa miaka 55, alikuwa rais wa kundi la FDLR baina ya mwaka 2008 na 2009, wakati waasi hao wakiendesha mapambano yao mashariki mwa Kongo.

Mwaka 2015, kiongozi huyo alitiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo cha miaka 13 jela na mahakama ya mjini Stuttgart kwa makosa ya kuongoza kundi la kigaidi na makosa mengine manne ya uhalifu wa kivita.

Hata hivyo, hukumu hiyo ilitenguliwa mwaka jana kutokana na makosa ya kisheria na kesi yake ilikuwa imepangwa kuendeshwa tena, huku akisalia kizuizini.

Mahakama hiyo ilisema kuwa afya ya Murwa-na-shyaka ilibadilika ghafla tarehe 11 mwezi huu, na siku chache baadaye alikufa akiwa hospitalini.

    

Post a Comment

0 Comments