WASOMI NA NDOTO ZA ABUNUASI

Hebu vuta picha,namna ulivyosota kuipata hiyo degree yako. Miaka isiyopungua 16 imeteketea darasani! Umebeba vidumu na ufagio kama wafagiaji wa jiji ukiwa shule msingi. Umepiga jaramba maili kadhaa kuifata shule.Umekumbana na kashkashi za walimu "wanoko",ukiwaona tu bandama zilikuwa zinacheza "ndombolo" na tumbo liliunguruma kama jenereta la kiwanda. 
Kasheshe ni pale ulipochaguliwa high school shule ya bweni! Enzi zile za ugali na maharage kama Segerea, wadudu ni wengi kuliko maharage! Hukukata tamaa ulivumilia kwa kuamini ipo siku tochi ya mafanikio itakumulika. 
Ukupigao ndio ukufunzao,ila hukujifunza pale ulipochaguliwa chuo! 
Masikini akipata....Boom lote liliyeyuka kwenye nguo! ulitaka na wewe ufanane na "watoto wa jiji"! Ulihudhuria disco zaidi kuliko lecture. Flat screen, "dance floor" vikahamia chumbani kwako! Suplimentary zikakukosa kosa, tia maji tia maji MUNGU si Athumani ukamaliza chuo na gamba lako! 
Wazazi wakawa na matumaini sasa ndio muda wa kula "pensheni" mana msomi umeshavaa joho! Umerudi chuo na rundo la makaratasi tu kama gari la magazeti!Yote hayo ukawaambia wazazi yanaitwa "madesa" na uliyasoma sana kumbe ulikuwa bingwa wa kuzima moto na "vizenga"(vibomu).Ulijulikana kama mzee wa "kujilipua". 
Mtaa ukakukaribisha kwa shangwe na vifijo.Haikupita wiki zile "Bata" za chuo ukaanza kuzimiss, daah! ulifulia hasa hata kifurushi uligongea cha bi mkubwa! Hizo zilikuwa salamu za rasharasha tu za kukukaribisha mtaani! 
Uliowacha ambao hawakuendelea na masomo, wapo mtaani, baadhi wamepauka kama kopa la mtwara, wengine "ngoma inogile" wanang'aa kama kikalio cha stova-wamewekeza kwenye biashara zao! 
Enzi zile uko chuo ulikuwa unawavalia miwani ya mbao na kujifaragua kama joka la mdimu kuwa si class yako utaongea nao nini? Sasa ndio wamekuwa wenyeji wako mtaani! Aibuuu!Umeshikwa na haya,sura imekushuka kama viraka ya nyongeza vilivyoisaliti suruali! 
Kila kazi unayoomba unaambulia usaili tu!Nyingine hata usaili hutii pua! kazi moja mnaitwa alfu tano! khaa! Ulidhani mlisoma "Survival for the fittest " ili mfaulu mtihani tu?ndiyo uko maabara sasa. 
Unazikumbuka pesa ulizozitumia "kula bata" chuoni,lol leo "bata" anakula wewe! "umeanza kuisoma namba" !Umepauka kama koti la mtunguo Tandika! 
Mungu si athumani ukabahatika ajira mpya huko kwetu "Nanjilinji". Mshahara laki 3,huna jinsi inabidi tu uende! Miaka mitatu sasa imepita huna tofauti na uliowakuta hapo "kijijini". Zile ndoto na hekaya za chuoni za kuwa na kazi ya 1.5M, ununue gari, ujenge nyumba, uwe na "demu" mkali,zoote zimeyeyuka kama samli kikaangoni! Magari unayaona mjini tu,"mademu" wakali unaendelea tu kuwaita "shemeji"! ndio hivyo, amtunzae mpiga zumari ndie anaechagua wimbo! Utatunza nini na wewe pangu pakavu tia mchuzi!sasa umekuwa mzee wa kaunda suti za kupauka kama inzi wa chooni. Gucci unaziona kwenye filamu tu ,wewe ni magauni ya chirimeni tu! 
Mjini unakuja mara moja kwa mwezi kufuata mshahara! Mwanzoni ulikuwa unaona taabu kukaa kijijini, kila weekend uko mjini, unajifanya alwatani "vascoda Gama", baada ya shida kukutandika vibao,sasa huna jeuri ya kupanda gari kila wiki! Hivi si ulisema ukimaliza chuo na kupata kazi utaunga kusoma masters?Vipi kwani vyuo vimefungwa? 
Haya ndio maisha ya vijana wengi! Hudhani mtaani kuna asali na maziwa wakishamaliza degree zao! Mtaani kuna hitaji zaidi ya hiyo degree!Kuna wakati degree inabidi uiweke pembeni ili ufunike kombe "mwanaharamu "apite!Lakini pia mtaa unakupokea kama ulivyojiandaa nao! kama kwa kutumia bumu lako ulijibana na kuhifadhi kidogo basi mtani utaziona fursa za kuwekeza hicho kidogo ulichonacho.Kama ulikula bata tu na mtaani umerudi na mawigi,kucha feki na "modo" za kuvaa mlegezo basi mtaa hautakuonea aibu, utakupa swaga zake.Nguo ya ijumaa hufuliwa Alhamisi#JIPANGE jombaaaaaaaaaa

Post a Comment

0 Comments