Auawa kwa Kuchomwa Kisu Akigombania Mwanamke Usiku wa Pasaka

 Mkazi wa Mji Mdogo wa Sirari tarafa ya Inchugu, wilayani Tarime mkoani Mara, Charles Mkono (26) ameuawa kwa kisu wakati wa usiku wa mkesha wa Pasaka.

Imeelezwa kuwa mtu huyo alichomwa kisu tumboni na mlinzi wa nyumba ya kulala wageni ya Mzalendo aliyejulikana kwa jina moja la Juma, mkazi wa Kitongoji cha Nyamorege Machinjioni kata ya Sirari, baada ya kutokea ugomvi unaosadikiwa ni wa kumgombea mwanamke.

Tukio hilo la kusababisha kifo kwa kijana huyo aliyefahamika kama DJ katika mji wa Sirari lilitokea usiku saa 2.

Nyumba ya kulala wageni ya Mzalendo ipo jirani na nyumbani kwao marehemu.

Watu walioshuhudia mkasa huo walisema kwamba wawili hao walikuwa wakimgombea mwanamke aliyetambuliwa kwa jina moja la Happy ambaye ilidaiwa alikuwa rafiki wa Mkono.

Diwani wa Kata ya Sirari, Nyangoko Paulo alisema tukio hilo la Mkono kuchomwa kisu tumboni na mlinzi lilitokea usiku saa 2 baada ya kukuta Happy akizungumza na mlinzi, jambo lililozua ugomvi.

Mkono alisikika akidai kuwa mlinzi huyo alikuwa anamfanyia mwanamke wake mpango kwa mtu mwingine aliyekuwa amelala katika nyumba hiyo ya wageni.

Kamanda wa Polisi Tarime, Rorya, Henry Mwaibambe alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema Jeshi la Polisi linamsaka mtuhumiwa. 

Post a Comment

0 Comments